Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi

NEC Logo

Tume yatangaza Uchaguzi Mdogo Jimbo la Amani na Kata 12 za Tanzania Bara kufanyika Desemba 17, 2022

Imewekwa: 10 Feb, 2023
Tume yatangaza Uchaguzi Mdogo Jimbo la Amani na Kata 12 za Tanzania Bara kufanyika Desemba 17, 2022

Tume ya Taifa ya Uchaguzi imetangaza Uchaguzi Mdogo wa Ubunge Jimbo la Amani katika Wilaya ya Mjini, Mkoa wa Mjini Magharibi, Tanzania Zanzibar na Madiwani katika Kata 11 za Tanzania Bara utakaofanyika tarehe 17 Desemba mwaka 2022.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Dkt. Wilson Mahera Charles, amesema katika taarifa kuwa uchaguzi huo umetokana na vifo vya Mbunge wa Jimbo la Amani na fivo vya madiwani na wengine kujiuzulu.

Dkt. Charles alifafanua kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ilipokea barua kutoka kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiitaarifu Tume kuwepo nafasi wazi ya Ubunge katika Jimbo la Amani kufuatia kifo cha mbunge wa jimbo hilo Mhe. Mussa Hassan Mussa (CCM) kilichotokea Oktoba 13, 2022.

Aliongeza kuwa aidha Tume ilipokea barua kutoka kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) akiifahamisha Tume kuwepo nafasi wazi za udiwani katika kata 12 kwenye halmashauri 11 za Tanzania Bara kutokana na vifo na kujiuzulu kwa madiwani.

“Kwa kuzingatia masharti ya Kifungu cha 37 (1) (b) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343 na Kifungu cha 13 (2) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292, Tume imeaandaa Uchaguzi Mdogo ili kujaza nafasi ya Ubunge Jimbo la Amani na nafasi za Udiwani katika kata 12 za Tanzania Bara” alisema Dkt. Charles.

Kwa mujibu wa ratiba ya uchaguzi huo Fomu za Uteuzi zitatolewa kuanzia tarehe 24 hadi 30 Novemba, 2022, Uteuzi wa Wagombea utakuwa tarehe 30 Novemba, 2022, Kampeni za Uchaguzi zitaanza tarehe 1 hadi 16 Desemba, 2022 na Siku ya Kupiga Kura itakuwa tarehe 17 Desemba mwaka 2022.

Dkt. Charles alitaja kata zitakazofanya Uchaguzi Mdogo wa Madiwani na halmashauri na mkoa yake kwenye mabano kuwa ni Kata ya Majohe (Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam-Dar es Salaam), Kata ya Dabalo (Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino-Dodoma) Kata ya Ibanda (Halmashauri ya Wilaya ya Kyela-Mbeya), na Kata ya Mndumbwe (Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba-Mtwara).

Kata ninyingine ni Kata ya Njombe Mjini (Halmashauri ya Mji wa Njombe-Njombe), Kata ya Misugusugu (Halmashauri ya Mji wa Kibaha-Pwani, Kata ya Dunda (Halmashauri ya Wilaya Bagamoyo-Pwani), Kata ya Kalumbeleza (Halamashauri ya Wialaya ya Sumbawanga-Rukwa), Kata ya Mwamalili (Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga- Shinyanga), Kata ya Mnyanjani (Halmashauri ya Jiji la Tanga-Tanga) Kata ya Lukozi (Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto-Tanga) na Kata ya Vibaoni iliyopo Halmashauri ya Mji wa Handeni Mkoa wa Tanga.